Huwa nadumu na imani, kinamama tukiondolewa mzigo huu, tunaweza!

By Tuntule Swebe , Nipashe
Published at 11:40 AM Apr 12 2024
Mwanamke kazini.
PICHA: MAKTABA
Mwanamke kazini.

JAMII ilikofika sasa, inapaswa kutambua kuwa mwanamke ana mhimili mkubwa unaowezesha gurudumu la maisha.

Wanawake wanapoamua pamoja, daima wanaweza. Hivyo, kinamama wanapaswa kuongoza watoto wa kike wenzao, waweze kutambua nafasi yao na kujua kilicho sahihi na kinachofaa katika maisha  na kipi hakistahili kuwa nacho.

Hivyo, wanaweza kufahamu mambo mbalimbali, ikiwamo anayopitia mwanamke katika umma unaomzunguka, hivyo watu  wote  kwa  ujumla  wanapaswa wakumbuke  nafasi ya mwanamke ilivyo katika jamii.

Ndani ya jamii za Kiafrika, zimekuwa na mtazamo  tofauti  kwa kinamama, kwa wanachokiamini kuwa mwanamke  ni mfanyakazi  za nyumbani  na  hana kitu kingine  cha  kufanya.

Hiyo, inawafanya baadhi ya kinababa wengi kutumia fursa  hiyo  kuwatumikisha  wanawake  bila  ya  huruma. Wanawake hawaruhusiwi kuwa na kauli sehemu yoyote. 

Mwanamke anashinda nyumbani, akitekeleza  majukumu  yote  na katika baadhi ya maeneo vijijini  tunasikia huko, Tarime  na Songea na vingine  vingi  hivyo  wanaume  walio  wengi wana watumikisha  wake  zao  bila  kujali  kama wamechoka  au  vinginevyo.

Majukumu yaliyozoeleka, yanajumuisha kukata kuni za mapishi, kuchota maji, hata wanaume ninawasihi peaneni elimu katika kuamini mwanamke,  ana haki  kwani  hata yeye  anachoka  hivyo  anatakiwa  kupumzika.

Hata   hivyo, bado  watu  walio  wengi  nadhani  elimu hiyo haijazama kwao kisawasawa,  kuna  baadhi  ya  makabila  yanayopenda  kurithi  wanawake, mila mbaya na iliyopitwa na wakati.

Ni jambo baya na si sahihi kumrithi mwanamke, kwani ni unyanyasaji  uliopitiliza na ni makosa  makubwa kisheria. 

Ni dhahiri katika hilo, anayehusika na tendo hilo anabaki kuwa mgandamizaji wa  haki  na  uhuru  wa kijinsia kwa mwanamke  husika, jambo  ambalo sio  la kiungwana na linakemewa vikali  

Hivyo, mwanaume anayefanya jambo hilo  la  kumrithi mjane,  anapaswa kuchukua  hatua,  kwani  sio  vyema. Naye, mwanamke anayo nafasi kubwa  katika  jamii  kwani, kinamama tunao  uhuru  wa  kushiriki  kwenye  kampeni  ikiwa  tunaelekea mwaka  wa uchaguzi huu 2024 na wa uchaguzi mkuu 2025.

Inatupasa na kukumbuka kwamba, tuna  nafasi  ya kuwa wazalendo katika kushiriki  kwenye uchaguzi  kikamilifu, kukiwapo maono  ya  kuwania  cheo. Kwa chochote kile, ni vyema mtu akajitambua anakoelekea. 

Wewe mama nakushauri, chukua fomu  za kuwania nafasi  bila  ya kuchelewa, hali itakayosaidia  ushindani  wa  hali  ya  juu  na  kuwafanya wanawake  kung’ara juu wakishika  nyazifa  za kuamua katika madaraka  ya nchi. 

Hivyo, nawasihi wenzangu, msiache kuwa  na  malengo  ya  kutimiza  ndoto  zenu, kwani kuna  baadhi  ya  wazazi  hasa  vijijini,  wamekuwa  na mtazamo tofauti  katika  malezi  ya watoto  wengi  wao, wakiamini  kuwa  mtoto  wa kike   hawezi  jambo  lolote la kufanya. Jambo hilo si la kweli hata  kidogo  tena!  

Kuna falsafa kwamba, mwanaume  ndiye  mwenye  haki  ya kurithi  na mengine mengi ya aina hiyo, jambo ambalo  sio la kweli.

Mimi naamini uhalisia, binti ana nafasi kubwa kuikomboa jamii hiyo inayomhusu. Mama huwa ana uthubutu, pale jamii ikimpa  haki na  uthubutu   wa  kujikomboa kuanzia na elimu.

Ni chanzo cha maendeleo na inatupasa kukumbuka kuna vyombo vinavyotetea haki za wanawake. 

Wanawake wana  fursa mbalimbali  za maendeleo,  kwani  hata  Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA),  kimeonyesha mfano kwa kutambulisha mradi mpya wanawake mnamo Oktoba, 2020.

Inatambua kuwa ushiriki wa wanawake katika  nafasi za maamuzi, hasa ya kisiasa, bado ni mdogo,  hivyo ina  azma ya kuwakwamua kushiriki kuwania nafasi mbalimbali za uongozi.

Bila shaka, hata watoto wa kike walioko shuleni wasome kwa bidii, kwani wanayo nafasi ya kuongoza  inahitaji elimu, hata kuwawezesha kuvuka katika malengo yao.

Niseme, bila ya kusahau napo wapo kinababa wanapaswa kupeana elimu ya utambuzi wa nafasi ya mtoto wa kike na kina mama kwa ujumla, taifa letu lizidi kuwa imara zaidi.